Goal.com
Live
1oegggny0kc9b1ojjpk2zgh55w

Rasmi: Yanga yaingia Mkataba na SportPesa

Hatimaye kampuni ya michezo ya kubashiri ya SportPesa imeingia mkataba wa miaka mitano na klabu kongwe Ligi Kuu Tanzania, Yanga.

Yanga inakuwa klabu ya pili kusaini mkataba na Kampuni hiyo kubashiri ya Kenya baada ya mahasimu wao Simba.

Miamba hao wa Jangwani wamevuna dau kubwa zaidi ya mahasimu wao, Simba SC katika udhamini wa kampuni ya SportPesa.

Wakati wiki iliyopita SportPesa ilitangaza kuingia mkataba wa miaka mitano na Simba kwa dau la Sh. Bilioni 4.96, leo imeingia mkataba wa kuidhamini Yanga kwa Sh. Bilioni 5 kwa miaka hiyo hiyo mitano.

Akizungumza wakati hafla ya kusaini mkataba huo makao makuu ya Yanga, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani mjini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi wa Utawala wa SportPesa, Tarimba Abbas alisama kwamba wameingia mkataba huko kwa dhumuni la kuendeleza soka katika kufikia malengo ya klabu hiyo.

Bw. Tarimba amesema fedha hizo zitatolewa kwa awamu, mwaka wa kwanza, Yanga watapata Sh. Milioni 950 na kama ilivyo kwa Simba, klabu ya Jangwani pia itatakiwa kuthibitisha matumizi ya fedha hizo kama yamefanyika kwa shughuli za maendeleo ya soka.

Alisema licha ya mkataba huo, pia kutakuwa na motisha ambapo wakishinda ubingwa wa Ligi Kuu watapewa zawadi ya Mill. 100.

“Pia ikishinda michuano kama Kagame pia watapewa zawadi na wakifanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa Afrika watapata zawadi ya Mil. 250,” alisema Tarimba.

Ukiondoa kuzidiwa kidogo kwa dau, lakini kwa ujumla mkataba huo hautofautiani sana na wa Simba.

Lakini kikubwa ni kwamba kwa mara nyingine, vigogo wa soka Tanzania na mahasimu wa jadi, Simba na Yanga wanatarajiwa kuwa chini ya udhamini mmoja tena, baada ya awali wote kudhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kati ya mwaka 2007 na 2016.

TBL iliachana na Simba na Yanga na kwa ujumla ilijitoa kwenye kudhamini soka, hadi timu ya taifa, Taifa Stars kufuatia mabadiliko ya umiliki wa kampuni hiyo.

Na miezi michache baada ya kupoteza udhamini wa TBL kupitia bia ya Kilimanjaro Premium Lager, hatimaye Simba na Yanga zitakuwa zinavaa jezi zenye kufanana tena maandishi kifuani, SportPesa.

Advertisement

ENJOYED THIS STORY?

Add GOAL.com as a preferred source on Google to see more of our reporting