Ratiba ya nusu fainali ya michuano ya Kombe la FA, imepangwa usiku wa kuamkia leo na sasa klabu ya Yanga itakutana na wababe wa Simba Coastal Union kwenye dimba la Mkwakwani Tanga, wakati Mwadui FC watapambana na Azam FC, uwanja wa Mwadui Complex Shinyanga mechi zote mbili zikipigwa Aprili 24,2016.
Lakini wakati Shirikisho la soka likitoa ratiba hiyo iliyorushwa live na kituo cha Televisheni cha Azam klabu za Yanga na Azam zimeomba mechi hizo zisogezwe mbele.
Sababu ikiwa ni mechi zao za CAF, ambazo wanatakiwa kucheza Aprili 20 ugenini na kurejea Dar es Salaam Aprili 21 usiku, hivyo watakuwa na muda mfupi kabla ya mechi za Kombe la FA ambazo watacheza ugenini pia.
Coastal Union iliingia hatua hiyo ya nusu fainali baada ya kuitoa Simba kwa kuifunga mabao 2-1, wakati Azam FC iliitoa Prisons kwa kuifunga 3-1, Mwadui FC iliitoa Geita Gold kwa kufunga 3-0 na Yanga iliwafunga Ndanda FC 2-1.
Bingwa wa Kombe la FA, mwaka huu, ataiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika 2017.
